Eunice Lumallas anayewakilisha magavana katika mahakama ya Masuala ya Nguvukazi iliyosema madaktari wamekiuka agizo; wataadhibiwa Desemba 22, 2016
Huenda maafisa wakuu wa chama cha kutetea madaktari (KMPDU) wakasherehekea sikukuu ya Krismasi jela endapo watafungwa Alhamisi na Mahakama ya kuamua mizozo ya wafanyakazi (ELRC) iliyowapata na hatia ya kukaidi agizo wasitishe mgomo ili wanachama wao warudi kazini.
HUENDA maafisa wakuu wa chama cha kutetea madaktari (KMPDU) wakasherehekea sikukuu ya Krismasi jela endapo watafungwa Alhamisi na Mahakama ya kuamua mizozo ya wafanyakazi (ELRC) iliyowapata na hatia ya kukaidi agizo wasitishe mgomo ili wanachama wao warudi kazini.
Jaji Hellen Wasilwa aliwaamuru maafisa wa kitaifa wa KMPDU wafike kortini Alhamisi kuadhibiwa kwa kukaidi agizo ‘madaktari warudi kazini’.
Jaji Wasilwa aliwapata maafisa hao wakuu wa KMPDU na hatia ya kukaidi agizo la Desemba 1,2016 aliyowataka “ madaktari warudi kazini.”
“Lazima maagizo ya hii mahakama yafuatwe. Wanaoyakaidi lazima waadhibiwe na hii mahakama kwa mujibu wa sheria,” akasema Jaji Wasilwa.
Ombi la CoG
Jaji huyo alikuwa ameombwa na wakili wa baraza la magavana (CoG) Bi Eunice Lumallas awasukume jela maafisa wa KMPDU kwa kukaidi agizo la mahakama.
“Maagizo ya hii korti sharti yafuatwe na kutekelezwa. Naomba hii korti iwapate na hatia maafisa wa kitaifa wa KMPDU kwa kukaidi agizo madaktari warudi kazini,” alisema Bi Lumallas.
Punde tu baada ya Jaji Wasilwa kuwapata na hatia maafisa hao wa KMPDU walisema kupitia kwa mawakili wao kwamba watakata rufaa kupinga agizo hilo.
Mgomo wa madaktari umeingia wiki ya tatu na wamedumisha msimamo kwamba lazima waongezwe mishahara kwa kiwango cha asili mia tatu.